Waziri mkuu wa Ethiopia amesema nchi yake "haitakubali vitisho vya aina yoyote" baada ya Rais Donald Trump kusema kuwa Misri inaweza kuharibu bwawa lenye utata la Nile.
Bwawa hilo kubwa linakabiliwa na mzozo unaohusisha nchi za Ethiopia, Misri na Sudan, Ambapo Rais Trump amesema Misri haiwezi kuishi bila bwawa hilo na huenda "ikalipua" ujenzi wa Bwawa hilo.
Haya yanajiri baada ya Marekani ilipotangaza mnamo mwezi Septemba kwamba itaipunguzia msaada Ethiopia baada ya nchi hiyo kuanza kujaza maji hifadhi iliyopo nyuma ya bwawa hilo mwezi Julai.
Misri, ambayo inategemea maji ya mto Nile kwa 80%, ina hofu kuwa bwawa hilo litaathiri mfumo wa usambazaji maji na kuifanya Ethiopia kuwa na mamlaka juu ya usambaaji wa maji ya mto mkubwa Afrika.
Ujenzi wa bwawa hilo la thamani ya dola bilioni nne mashariki mwa Ethiopia utakuwa mradi mkubwa zaidi wa umeme barani Afrika.
Mzozo wa bwawa la mto Nile wazua cheche za maneno kati ya Ethiopia na Misri
Sudan, ambayo inapakana na Misri upande wa juu pia inahofia kupunguziwa maji.
Ethiopia, ambayo ilitangaza ujenzi wa bwawa hilo mwaka 2011, inasema kuwa inataka kutumia maji ya bwahilo kujiendeleza kiuchumi.
Ujenzi huo ulianza mwaka 2011 kaskazini mwa Ethiopia ambapo maji yatakayotumika ni 85% ya maji yanayotiririka kutoka mto Nile.
Hata hivyo ujenzi huo umesababisha kuwepo kwa mzozo kati ya Misri na Ethiopia, huku Sudan pia ikihusishwa na sasa Marekani inajaribu kutatua mzozo huo, Lakini sasa majadiliano yanasimamiwa na Muungano wa Afrika.
"Ethiopia haitakubali vitisho vya aina yoyote," alisema. "Waethiopia hawajawahi kupiga magoti mbele ya maadui wao, lakini wanawaheshimu marafiki zao. Hatutafanya hivyo wala siku zijazo."- Waziri Mkuu Abiy Ahmed
Aidha, inaelezwa kuwa kuna hofu kwamba hatua ya Ethiopia kuanza kujaza maji bwawa hilo huenda ikalemaza matumaini ya kusuluhisha masuala muhimu, kama vile kitachotokea wakati wa ukame na jinsi ya kusuluhisha mizozo ya baadaye.