Katika kipindi cha miezi sita, katika mkoa wa Ituri, zaidi ya watu 1,800 wameuawa huku 1,600,000 wameyatoroka makazi yao, shule 300 zimeharibiwa katika mkoa wa Ituri, kulingana na Radio ya Umoja wa Mataifa nchini DRC, OKAPI, ikimnukuu mbunge Jackson Ausse.
Idadi hii imewekwa wazi na Mbunge wa kitaifa Jackson Ausse, katika barua ya wazi iliyotumwa Jumanne, Septemba 22 kwa Rais Felix Antoine Tshisekedi.
Barua hiyo ya Mbunge Jackson Ausse imezungumzia kuongezeka kwa athari za kibinadamu zinazosababishwa na ukosefu wa usalama katika mkoa wa Ituri tangu mwezi Machi mwaka huu.
Katika kukabiliana na hali hii ya usalama na hali ya kibinadamu, Mbunge Jackson Ausse amemuom Rais Felix Tshisekedi kutangaza hali ya dharura ya usalama katika katika mkoa wa Ituri hili na vilevile katika mkoa wa Kivu Kaskazini.
Hayo yanajiri wakati mapigano ya kikabila katika mkoa wa Kasai nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, yamesababisha vifo vya watu 11 na wengine zaidi ya Elfu 10 kuyakimbia makazi huku nyumba zaidi ya Elfu moja yakiteketezwa moto, katika mapigano hayo yaliyotokea mapema mwezi huu.
Ripoti ya Shirika lisilokuwa la kiserikali la Kanisa Katoliki CARITAS,limesema mapigano hayo yalianza Septemba 05, na kuendelea kwa siku tatu mfululizo.
Shirika hilo la Kanisa Katoliki linatarajiwa kuzuru eneo hilo, kujionea hali ilivyo baada ya mapigano hayo ambayo pia yaliwahi kuzuka kati ya ya mwaka 2016 na 2017 na kusababisha maafa.
Mkoa wa Kasai umeendelea kushuhudia ukosefu wa usalama kwa karibu miaka miwili sasa baada ya maafisa usalama kumuua Kamuina Nsapu kiongozi mkubwa wa kijamii.
Tangu Septemba mwaka 2016 na mwezi Oktoba mwaka 2017 watu zaidi ya Elfu tatu walipoteza maisha katika eneo hilo, huku wengine zaidi ya Milioni 1 na Laki Nne wakiyakimbia makazi yao.