Muungano wa wanahabari nchini Burundi, umetoa wito kwa rais Évariste Ndayishimiye kuwasamehe wanahabari wanne wa Gazeti binafsi la Iwacu, waliofungwa jela kwa kosa la kutishia usalama wa nchi hiyo.
Waandishi hao walishtumiwa kosa hilo walipokwenda kuripoti mapigano kati ya wanajeshi na kundi lenye silaha, katika Mkoa wa Bubanza mwaka uliopita.
Mapema mwezi Juni mwaka huu Mahakama ya Rufaa nchini Burundi ilipitisha hukumu ya miaka miwili iliyotolewa kwa waandishi hao ambao walikuwa walihukumiwa katika mahakama ya mwanzo kwa makosa ya kuhatarisha usalama wa taifa.
Waandishi hao ni wafanyakazi wa shirika la habari la Iwacu ambalo ni moja kati ya mashirika machache binafsi katika taifa hilo.
Waandishi hao wanne waliohukumiwa, walikamatwa mnamo mwezi Oktoba mwaka uliopita katika eneo la Musigati, mkoani Bubanza, huku vituo kadhaa vya redio na vyombo vingine vya habari vilifungwa na waandishi wengi wa habari waliikimbia nchi hiyo.
Kamati ya Kuwalinda Wanahabari (CPJ) na mashirika mengine 80 ya kutetea haki za wanahabari na haki za kibinadamu hivi majuzi walituma barua kwa viongozi wa nchi za Afrika, kuwahimiza kuwaachia huru wanahabari wote wanaozuiliwa kwa kuzingatia mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19.