Serikali imetangaza kuanzia tarehe 01 hadi 08 Agosti, 2020 kutafanyika maadhimisho ya sikukuu ya wakulima Nanenane ambapo kitaifa yatafanyika katika viwanja vya Nyakabindi, Wilaya ya Bariadi Mkoani Simiyu.
Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga amesema kuwa Maonesho hayo yataambatana na uhamasishaji wa matumizi ya teknolojia bora za kilimo, ufugaji na uvuvi. Pia, maonesho hayo yatashirikisha Wadau mbalimbali zikiwemo Wizara, Taasisi za Umma na Binafsi, Wabia wa maendeleo, wakulima na Vyama vya wakulima, wafugaji na wavuvi.
Mhe Hasunga amesema kuwa Kupitia Maonesho hayo, Viongozi mbalimbali wa Kitaifa watatembelea viwanja vya Maonesho na kuhamasisha masuala mbalimbali ya kuendeleza sekta za kilimo, mifugo, uvuvi pamoja na Ushirika.
Amewataja baadhi ya Viongozi wanaotarajiwa kushiriki katika Maonesho hayo ngazi ya Taifa ni Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kadhalika amelitaja Lengo la Maonesho ya Nanenane katika kanda hizo kuwa ni pamoja na kutoa fursa kwa wakulima, wafugaji, wavuvi na wanaushirika kuona na kujifunza matumizi ya teknolojia bora za kilimo, ufugaji na uvuvi kwa ajili ya kuongeza tija na uzalishaji kwa uhakika wa chakula, kukidhi mahitaji ya viwanda na masoko ya ndani na nje ya nchi.
Kaulimbiu ya Maonesho hayo kwa Mwaka huu ni kauli mbiu isemayo “Kwa Maendeleo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi Chagua Viongozi Bora 2020“.
Maonesho hayo ya 28 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1993 yatafanyika kwenye Kanda nane (8) za Maonesho ambazo ni Kanda ya Mashariki (Morogoro), Kanda ya Kaskazini (Arusha), Kanda ya Magharibi (Tabora), Kanda ya Kusini (Lindi), Kanda ya Kati (Dodoma), Kanda ya Nyanda za Juu Kusini (Mbeya), Kanda ya Ziwa Mashariki (Simiyu) na Kanda ya Ziwa Magharibi (Mwanza).