Aliyewahi kuwa Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) amejiunga Chama cha Mapinduzi (CCM).
Akizungumza katika mkutano wa kupokelewa na viongozi wa CCM Mkoa wa Arusha Nassari amesema kuwa amejiunga chama hicho ili kujiweka katika upande mmoja na wale wanaoitakia nchi hii maendeleo.
"Wengine wanasema Nassari anautaka Ubunge, niwaambie sijatangaza nia mahali popote na sijaja CCM kutangaza nia, nimetafakari pia Jamii, Wazee wa Meru na Marafiki waliofanya nikawa Mbunge mdogo kuliko wote Nchi hii wameniambia, naona CCM huku kunafaa, Haikuwa kazi rahisi kufanya haya maamuzi ya kuja CCM, yale yote mnayotaka kuyasikia na kuyaona kutoka kwangu mtayasikia na kuyaona hata kama sio leo, sababu kubwa iliyonileta CCM ni kuwa naipenda Nchi yangu”.
Nassari amesema ameamua kuiweka Nchi yake mbele, haijalishi watu wapo watakaomtukana au watakaosema hili na lile kuhamia kwake kwenye chama hicho lakini haitamrudisha nyuma, zaidi ya kuwashukuru Watu wa Meru kwa kumuamini kwa mihula miwili mfululizo nikiwa Mbunge mdogo kuliko wote hapa nchini.
“Watanzania wanaokwazwa kwa kuona nimeingia CCM ambao walitamani kuendelea kuniona upinzani naomba mnisamehe, siwezi kuendelea kuwa mnafiki roho yangu imekataa, sijatangaza nia na huenda nisichukue fomu, mkisema tunataka tukupe sehemu hayo tutaongea baadaye”-Alisema Nassari.
Aidha, Nassari amesema amekuwa akifanya siasa za kiungwana siku zote na tayari ameshaandika barua kwa uongozi wa CHADEMA; Kiukweli naishukuru CHADEMA ilinichukua nikiwa mdogo wakanisikiliza wakaona kuna potential ndani yangu, nawashukuru kwa kunilea nitakuwa mjinga kama sitoikumbuka historia”-Joshua Nassari.
Nassari ameongeza kuwa serikali ya Rais John Magufuli imefanya mambo mengi ambayo amekuwa akiyapigania kama vile kuboresha elimu, huduma za afya na ujenzi wa miundombinu pamoja na kuiwezesha Tanzania kufikia uchumi wa kati, hivyo hakuna sababu yoyote ya kumpinga.
Joshua Nassari alivuliwa ubunge wake Machi 2019 kutokana na kutohudhuria mikutano mitatu ya bunge mfululizo bila ruhusa, kitendo ambacho ni kinyume na sheria.