Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema ameridhishwa na maendeleo na kasi ya ujenzi wa mabehewa mapya kwa ajili Reli ya Kisasa (SGR) ya Shirika la Reli Tanzania yanayotengenezwa na kampuni ya Sung Shin Rolling Stock (SSRT) iliyoko nchini Korea Kusini.
“Kati ya mabehewa 81 ambayo Tanzania inatengeneza kutoka kwenu, tayari 36 yamekamilika na yameshapelekwa nchini Tanzania na 45 yaliyobaki yanategemewa kukamilika Machi, 2023. Mabehewa haya ni ya daraja la tatu na yatatoa huduma zote muhimu.”
Kadhalika, Waziri Mkuu amemkaribisha nchini Rais wa Kampuni hiyo Gye Shul Park aje kuwekeza nchini Tanzania kutokana na fursa mbalimbali zilizopo ikiwemo mpango wa Serikali wa kuendelea kuiboresha sekta ya usafiri wa reli.
Aidha, Majaliwa alitembelea kituo cha Seamul Undong ambacho ni taswira ya maendeleo ya Korea kupitia mpango wa kuviwezesha vijiji ambao unatekeleza mpango huo nchini Tanzania katika mkoa wa Morogoro (Pangawe).