Waumini wa Dini ya Kiislamu nchini wametakiwa kuendelea kuyaenzi mafundisho ya mtume Muhamad S.A.W yanayojikita katika upendo, mshikamano na amani ili jamii na Taifa kwa ujumla liweze kufikia maendeleo yaliyokusudiwa.
Akihutubia katika kilele cha siku kuu ya Maulid Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa wito kwa waumini wa dini ya kislam kuendelea kuyaenzi mafundisho ya mtume Muhamad yanayosisitiza upendo, Amani na mshikamano.
Waziri Mkuu amesema Serikali imeonesha kwa vitendo kuongoza Taifa na kufikisha maendeleo kwa Watanzania wote bila kujali tofauti za kidini na ukabila.
Majaliwa amesema kuwa Serikali imeendelea kusimamia mshikamano, haki na umoja wa Taifa, hivyo amewasihi Watanzania wote waendelee kumuombea Rais Samia ili aendelee kuiongoza vyema nchi yetu.
Ameyasema hayo leo Jumanne (Oktoba 19, 2021) alipomuwakilisha Rais Samia katika Baraza la Maulid lililofanyika Kitaifa katika uwanja vya Kaitaba mjini Bukoba Mkoani Kagera.
Waziri Mkuu amewataka waumini wa dini ya Kiislam nchini watumie maadhimisho hayo kama fursa muhimu kwao kuyasoma na kuyatafsiri kivitendo maisha ya Mtume Muhammad (S.A.W) katika mfumo wao wa maisha ya kila siku.
“Tafakuri hiyo ituwezeshe kuishi maisha ya undugu, kupendana, kuheshimiana na kushikamana miongoni mwetu Waislam pamoja na Watanzania wote kwa ujumla.”
Akizungumzia suala la amani na utulivu Majaliwa amesema kuwa amani ni tunu adhimu ambayo Mwenyezi Mungu ametukirimia kwani kuishi kwa amani ni kumfanya ibada Mwenyezi Mungu.
“Kudumisha amani iwe ni wajibu wa kila mmoja wetu kwani amani ndiyo kila kitu. Bila amani hatuwezi kupata maendeleo, hatuwezi kufanya ibada, watoto wetu hawawezi kwenda shule na mambo mengine mengi”.
Ameongeza kuwa Tanzania imekuwa kinara katika kuenzi na kudumisha amani, hivyo ni wajibu wa kila Mtanzania kuendelea kuitunza amani hiyo kwa kuwafundisha vijana na watoto misingi ya amani ili nao waidumishe.
“Serikali inatambua umuhimu wa madhehebu ya dini katika kudumisha amani. Viongozi wa dini mmekuwa mabalozi wema na kudumisha amani yetu kwa miongo kadhaa. Jitihada zenu zote zimewezesha nchi yetu kupata utulivu kila wakati na aghalabu kuwa kimbilio la majirani pindi wanapopata machafuko.”
Kadhalika, Waziri Mkuu Majaliwa ametumia fursa hiyo kuwasihi viongozi wa dini kuwaelimisha waumini wao kufanya maandalizi kwa ajili ya kushiriki katika zoezi la sensa ya watu na makazi ambayo inatarajiwa kufanyika Agosti mwakani.