Katika kuadhimisha Siku ya Kichaa cha Mbwa Duniani kila mwaka ifikapo tarehe 28 ya kila mwezi Septemba, Wizara ya Afya imewatahadharisha wananchi kujikinga na ugonjwa huo hatari ambao unaweza kusababisha vifo.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Msaidizi Magonjwa Yasiyo ambukiza Dkt. James Kiologwe akitoa Tamko la Serikali kwa niaba ya Katibu Mkuu katika kuadhimisha siku ya ugonjwa huo Duniani.
“Kwa mwaka huu kati ya mwezi Januari hadi Agosti, watu 39,787 wametolewa taarifa ya kung’atwa na mbwa au wanyama wa jamii hiyo ikiwa ni ongezeko la zaidi ya watu 5,000 ukilinganisha na kipindi kama hicho cha mwaka uliopita” -Amesema Dkt. James Kiologwe
Aidha, Dkt. Kiologwe ameitaja Mikoa inayoongoza kuwa ina idadi kubwa ya wagonjwa ni Mkoa wa Morogoro ambao una wagonja 4329 ukifuatiwa na Mkoa wa Dodoma wenye wagonjwa 4233.
“Waathirika wakuu wa ugonjwa huu ni watoto chini ya miaka 15 na hii inaweza kuwa ni kwa sababu wao ndio wanaokuwa karibu na mbwa (anayefugwa) muda mwingi, na pia hupenda kucheza au kuchokoza mbwa wasiowafahamu njiani” amesema Dkt. Kiologwe.
Dkt. James amesema kuwa Ugonjwa wa kichaa cha mbwa husababishwa na Kirusi wa Kichaa cha Mbwa (Rabies Virus) kutoka kwa wanyama jamii ya mbwa ambao wameathirika na kirusi hiki (Mbwa, paka, mbweha, fisi na wengineo) na humwingia mwanadamu kupitia mate ya mnyama huyo kuingia katika jeraha na dalili huanza kuonekana baada ya kuathirika kwa mfumo wa kati wa fahamu.
“Endapo mtu ameng’atwa na mbwa, hatua ya kwanza muhimu ni kuosha jeraha kwa dakika 10 au zaidi kwa maji mengi yanayotiririkika na sabuni. Kidonda kisifungwe na kisha apelekwe au afike haraka katika kituo cha kutolea huduma za afya ili kupata chanjo ya kuzuia kichaa cha mbwa”-Amesema Dkt. James Kiologwe.
Amesisitiza kuwa ni muhimu aliyeng’atwa na mbwa afanyiwe tathmini ya kina katika kituo cha kutolea huduma ili aweze kupatiwa chanjo kamili na iwapo chanjo itatolewa ni budi kumaliza kozi zote za chanjo.
Amesema kuwa Wizara ya Afya kwa kushirikia na sekta nyingine ikiwemo Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ofisi ya Waziri Mkuu (OWM) - Dawati la Afya Moja pamoja na Shirika la Afya Duniani (WHO), Shirika la Chakula Duniani (FAO) pamoja na wadau mbalimbali wamefanya juhudi mbalimbali za kudhibiti ugonjwa huo na kuhakikisha inapunguza ukubwa wa tatizo linalohusiana na ugonjwa huo.