Kamati ya Haki, maadili na madaraka ya bunge ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imemkuta na hatia Mchungaji na Mbunge wa jimbo la Kawe Josephat Gwajima ya kutoa taarifa za uongo kuhusu chanjo za corona.
Mwenyekiti wa Kamati ya haki, maadili na madaraka ya bunge, Emmanuel Mwakasaka amesema kauli zilizotolewa na Gwajima zimedhalilisha nafasi ya mbunge, zinashusha heshima ya bunge, wabunge na viongozi, zinachonganisha mhimili wa bunge dhidi ya muhimili wa serikali, serikali na wananchi na bunge na wananchi.
''Kauli za Josephat Gwajima zinagonganisha, zinachonganisha na kufarakanisha serikali na wananchi kwa kuwaaminisha kuwa serikali inawalazimisha wananchi kuchanjwa wakati jambo hilo ni la hiyari.''
Mwenyekiti wa Kamati hiyo aliongeza kuwa, ''Kwa kauli kwamba anayekubali chanjo amepokea pesa kutoka nje ya nchi na kampuni zinazotengeneza chanjo ni jambo linalotafsiriwa kuwa rushwa, kauli hizi zinaathiri mahusiano kati ya nchi yetu na nchi nyingine, jambo hili ni dosari kwa kiongozi anayetumia nafasi ya mbunge''.
Mwenyekiti Mwakasasa amesema Mch. Gwajima hajutii kauli zake na kwamba ataendelea kutoa kauli na kusisitiza kuwa huo ndio msimamo wake, imani yake na majibu yake yalikuwa yamejikita katika kueleza kuwa kamati haina mamlaka ya kuhoji mahubiri yake ya kanisani.
Aidha Kamati imependekeza Gwajima apewe adhabu kutohudhuria mikutano miwili mfululizo ya Bunge, na pia imetaka serikali ifuatilie matamshi na matendo yake kwani kuna uwezekano wa jinai ndani yake.