Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewataka Makatibu Tawala wa mikoa pamoja na wakuu wa taasisi wateule walioapishwa kwenda kufanya kazi kwa kuzingatia juhudi, maarifa, sheria na utu ili kutimiza matarajio ya wananchi kutoka kwa serikali.
Rais Samia ametoa kauli hiyo katika hafla ya kuwaapisha Makatibu Tawala wa Mikoa pamoja na viongozi wa taasisi ambapo wataka viongozi hao kutimiza majukumu yao kikamilifu ikiwa ni pamoja na kusimamia vema mapato ya halmashauri.
"Nyinyi ni wasimamizi wa shughuli zote za kiutendaji katika mikoa yenu, kwahiyo mna kazi kubwa ya kwenda kuifanya huko muendako, hii maana yake ni kwamba viongozi wote wa serikali wako chini yenu...zaidi ya hapo nyinyi ni kiungo muhimu kati ya serikali za mitaa na serikali kuu, MADED wote nyinyi ndio viongozi wao, wanakutazameni nyinyi mna kazi kubwa ya kwenda kufanya ikiwemo ya kusimamia mapato"- Rais Samia.
Kwa upande wake Makamu wa Rais ametoa rai kwa viongozi hao kutumia uzoefu wa viongozi waliowatangulia kwa kusikiliza kero za wananchi pamoja na kuzitatua.
Aidha, Waziri Mkuu Kassimu Majaliwa amewakumbusha Makatibu Tawala kwa kuwasihi kuwa wao ndio wenye jukumu kubwa la kuhakikisha miradi ya serikali inakamilika kwa ajili ya kufikisha huduma nzuri kwa wananchi.
Hafla hiyo ya kuwaapisha Makatibu Tawala wa Mikoa kumi na moja imehudhuriwa na Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Naibu Spika wa Bunge pamoja na viongozi wengine wa serikali.