Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Jumatatu alitangaza baraza jipya la Mawaziri katika hatua ambayo inaimarisha udhibiti wa Rais Felix Tshisekedi serikalini.
Serikali mpya ya muungano ina mawaziri 57 wakiwemo wanawake 14, huku 10 tu ndio kutoka Baraza la Mawaziri lililopita.
Huu ni muungano mpya wa Rais Tshisekedi uliotangazwa tarehe 6 Disemba baada ya kuvunja ushirikiano wake na Rais wa zamani Joseph Kabila.
Waziri Mkuu Jean-Michel Sama Lukonde, ambaye aliteuliwa mwezi Februari, amemtaja mchumi Nicolas Kazadi kuwa Waziri wa Fedha, Mwanaharakati wa zamani wa asasi za kiraia Antoinette N'Samba Kalambayi kuwa Waziri wa Madini na Jenerali Mstaafu Daniel Aselo Okito kuwa Waziri wa Mambo ya ndani, kwa mujibu wa ripoti ya shirika la habari la Reuters.
Shirika la habari la AFP limesema kuwa takwimu kutoka kwa wapinzani wa Kabila wameteuliwa kwenye nafasi muhimu, wakiwemo Waziri wa Mazingira na Naibu Waziri Eve Bazaiba wa chama cha upinzani cha Movement for Liberation of the Congo (MLC).
Christophe Lutundula, Waziri mpya wa Mambo ya nje, yuko karibu na Gavana wa zamani wa Katanga Moise Katumbi.
Rais wa zamani Kabila bado alikuwa akishika madaraka makubwa hata baada ya kuachia ngazi kufuatia uchaguzi wa 2018 - kwani muungano wake ulikuwa umeshinda viti vingi vya ubunge.
Mnamo Disemba, Rais Tshisekedi aliamua kuvunja muungano na Rais aliyekuwa mtangulizi wake Bwana Kabila na kulazimisha kujiuzulu kwa Waziri Mkuu.
Chanzo:BBCSwahili