Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema tayari serikali imekamilisha malipo ya ununuzi wa ndege mpya tatu.
Waziri Mkuu Majaliwa amethibitisha hilo wakati akitoa hoja bungeni juu ya makadirio na matumizi ya fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Ofisi ya Bunge kwa mwaka wa fedha 2021/2022.
Majaliwa amesema kuwa ndege hizo zinatarajiwa kuwasili katika kipindi cha mwaka wa fedha 2021/22 na hivyo kuwezesha serikali kuwa na ndege zake 12.
Waziri Mkuu Majaliwa amepongeza shirika la Ndege la ATCL kwa kuanzisha safari za kwenda nje ya nchi Guangzhou China, akisema kuwa safari hizo ni chachu ya kuimarisha biashara, utalii na ajira.
Kauli hii imekuja baada ya Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali nchini Tanzania, Charles Kicheere, kutoa ripoti yake juma lililopita kueleza changamoto zinazolikabili shirika hilo la ndege.
CAG alisema Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) limeingiza hasara ya takribani Shilingi Bilioni 150 kwa miaka mitano iliyopita.
Katika upande mwingine Waziri Mkuu Majaliwa ameliomba Bunge kuidhinisha zaidi ya Shilingi Bilioni 245.5 kwa ajili ya ofisi hiyo, taasisi zilizo chini yake na mfuko wa bunge ili kufanikisha utekelezaji majukumu mbalimbali.
Mjadala wa bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizochini yake utajadiliwa kwa siku nne na wabunge kisha serikali kuja na majibu ya hoja mbalimbali zitakazoibuliwa na wabunge.