Jeshi la Msumbiji linasema kuwa limeukomboa mji wa Pwani wa Palma, ikiwa ni wiki moja toka ulipotekwa na wanamgambo wa Kiislamu.
Maelfu ya watu wameukimbia mji wa Palma toka wanamgambo walipovamia mji huo mwishoni mwa mwezi uliopita.
Msemaji wa Jeshi ameeleza kuwa idadi kubwa ya wanamgambo wameuawa katika shambulio la kuukomboa mji huo.
Radio ya taifa hilo imeripoti kuwa wakazi waliokumbia mji huo wameanza kurejea huku baadhi wakikuta nyumba zao zikiwa zimeporwa vilivyomo.
Makumi ya raia waliuawa huku zaidi ya 11,000 wakilazimika kuyakimbia makazi yao baada ya wanamgambo hao kuvamia mji huo Machi 24, Mawasiliano baina ya mji huo wenye wakaazi 75,000 na sehemu nyingine za nchi bado hayapo.
Wanamgambo hao ambao wanafahamika na wenyeji wa Cabo Delgado kama al-Shabab ni wafuasi wa kundi la kigaidi la Islamic State (IS).
Shambulio hilo limeilazimu kampuni kubwa ya mafuta ulimwenguni Total kusimamisha mradi wa mabilioni ya dola wa gesi asilia katika eneo la Afungi, umbali mfupi kutoka mji wa Palma.
Msemaji wa jeshi, Brigedia Chongo Vidigal amesema mtambo wa gesi upo salama na mji wa Palma pia upo salama.
Gavana wa Cabo Delgado, Valgy Tauabo, alizuru Palma siku ya Jumapili na kuahidi kusaidia wakaazi kuyajenga tena maisha yao.
"Kwa sasa tunahamia katika hatua inayofuata, hatua muhimu zaidi, ambapo tutawakaribisha wakaazi ambao walikimbilia msituni,"- ameeleza Brig. Vidigal.
Aidha Maelfu ya wakazi wengine waliukimbia mji huo kwa mashua kuelekea katika makao makuu ya jimbo hilo, mji wa Pemba.