Hatimaye aliyekuwa Rais wa awamu ya tano Hayati Dkt. John Pombe Magufuli amezikwa katika makazi yake eneo la Mlimani Chato leo Machi 26,2021.
Shughuli hiyo ya maziko iliyofanyika katika makaburi ya familia ya marehemu ilihusisha watu wachache wakiwemo viongozi wa serikali, wastaafu pamoja na familia yake.
Maelfu ya Watanzania wameshuhudia tukio hilo moja kwa moja kupitia vyombo vya habari vilivyokuwa vinarusha shughuli hiyo ya mazishi.
Rais wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan katika hotuba yake amesema: "Tunashukuru sana katika uongozi wake tumejifunza mengi, tumepikwa vizuri, tumeivaa haswa na tumeuiva sawa sawa. Tunapokwenda kumpumzisha tunaweza kusema bila kigugumizi, kuwa tuko tayari kuendeleza kazi yake nzuri kwa nguvu, kasi na ari ile ile."
Kwa upande wake Mkuu wa Majeshi ya Tanzania, Jenerali Venance Mabeyo ameahidi utiifu kwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu Samia Suluhu Hassan.
Jenerali Mabeyo amemhakikishia Rais Samia Suluhu Hassan kuwa ulinzi wa nchi na mipaka yake ni salama na vitaendelea kumlinda, kumtii kama Amiri Jeshi Mkuu na kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa katiba ya Tanzania.
"Tunakuahidi utiifu, uadilifu na uaminifu mkubwa kama ilivyo ada ya mila na desturi ya majeshi yetu katika awamu zote zilizopita kwa manufaa ya ulinzi, usalama na ujenzi wa taifa letu’’- Amesema Jenerali Mabeyo.
Aidha, jenerali mabeyo ameelezea namna alivyomfahamu pamoja na kufanya kazi na hayati Rais Dkt. Magufuli.
‘’Aliviamini na kuvipenda vyombo vya ulinzi na usalama alihakikisha kuwa anaviwezesha kwa mahitaji ya kiutendaji na utawala ili viweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na weledi mkubwa, alisema hatuwezi kuwa na vyombo vya ulinzi imara bila kuwa na uchumi madhubuti, hatuwezi kutegemea misaada ya kuimarisha vyombo vyetu lazima tuimarishe uchumi wetu ili tuweze kuimarisha vyombo vyetu vya ulinzi na usalama’’-Jenerali Mabeyo.
Rais Dkt. Magufuli alifariki Machi 17, 2021 katika hospitali ya Mzena jijini Dar es Salaam kwa maradhi ya moyo.