Rais wa Tanzania John Magufuli hii leo Februari 19,2021 ameongoza waombolezaji katika kuaga mwili wa Katibu Mkuu Kiongozi John Kijazi.
Shughuli hiyo imefanyika katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es salaam, na imehudhuriwa baadhi ya watu wakiwemo wanafamilia na viongozi wa serikali.
Aidha, Baada ya shughuli hiyo ya kuaga kumalizika mchana wa leo kwa taratibu za kiserikali, mwili unategemewa kusafirishwa hadi Korogwe mkoani Tanga ambapo ndipo atazikwa hapo kesho Jumamosi.
Katika hotuba yake amewataka Watanzania kuacha kutoa taarifa za uongo kuhusu vifo vya viongozi ilihali wako hai hali inayozua khofu kwa wengi.
“Leo nimetumiwa meseji na Waziri wa Fedha Dr. Mpango ambaye amelazwa Dodoma, na ninaoomba niisome hapa kwa faida ya waliokuwa wanatweet kwamba amekufa, anasema;......Mhe. Rais naendelea vizuri, ninakula, ninafanya mazoezi ya kifua na kutembea, wanaonizushia kifo mitandaoni niliwaombea msamaha kwa Yesu Jana katika sala ya jioni’, ni huyo ambaye walisema amekufa, yeye aliwaombea msamaha kwa Yesu.'.... Magonjwa yapo tu, Mungu hashindwi, tulishinda mwaka jana, inawezekana hili ni jaribu jingine, tusimame na Mungu tutashinda"-Rais Dkt.John Magufuli akiwa Karimjee.
Kabla ya kuwa balozi, Mhandisi Kijazi alikuwa Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi na baadaye Wizara ya Maendeleo ya Miundombinu kuanzia mwaka 2002 hadi 2006, baada ya kuteuliwa kuwa Balozi ndani ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano waKimataifa na hatimaye kupangiwa kituo cha New Delhi, India.
Balozi Mhandisi John William Herbert Kijazi amekuwa mwakilishi wa Tanzania nchini India, Singapore, Sri Lanka, Bangladesh na Nepal mwenye makazi yake jijini New Delhi, India kuanzia mwaka 2007 - 2016 na hivyo kumfanya kuwa Mkuu wa Mabalozi wote wanaowakilisha Tanzania nje ya nchi.
Balozi Kijazi alifikwa na umauti Februari 17,2021 majira ya saa tatu usiku katika hospitali ya Benjamin Mkapa Jijini Dodoma ambako alikuwa akipatiwa matibabu.