Kiongozi wa upinzani Robert Kyagulanyi maarufu Bobi Wine, amemtaka jaji Mkuu kujiondoa katika kusikiliza shauri la kupinga kuchaguliwa tena Rais Yoweri Museveni.
Bobi Wine amemshutumu jaji Alfonse Owiny - Dollo kwa upendeleo kwa sababu ya ushirika wake na rais wa Uganda, Yoweri Museveni.
Mwanasiasa huyo wa upinzani pia anataka majaji wengine wawili wa mahakama ya juu kujiondoa kusikiliza shauri hilo kwa misingi hiyohiyo.
Majaji watatu hawajajibu chochote kuhusu shutuma dhidi yao.
Jaji Mkuu Owiny-Dollo alikuwa mwanasheria wa Rais Museveni mwaka 2006, kwa mujibu wa tovuti ya Nile Post.
Jaji Mike Chibita alikuwa msaidizi wa Museveni katika masuala ya sheria, wakati Jaji Ezekiel Muhanguzi ni ndugu wa Waziri wa Ulinzi Elly Tumwine kwa mujibu wa vyombo vya habari vya nchini humo.
Bobi Wine amedai kuwa watatu hao hawataweza kutenda haki iwapo watasikiliza shauri hilo.