Mahakama ya kijeshi jijini Kampala Uganda kwa mara ya pili imekataa rufaa ya wafuasi 36 wa chama cha upinzani cha National Unity kinachoongozwa na Robert Kyagulanyi maarufu Bobi Wine.
Miongoni mwa watu hao ni mlinzi binafsi wa Bobi Wine ajulikanaye kwa jina la Edward Ssebufu, na mshirika wake Ali Bukeniare ambao wanakabiliwa na mashtaka ya kukutwa na risasi.
Walikamatwa mwezi Desemba mwaka jana wakati wa kampeni za kuwania urais za Bobi Wine katikati mwa wilaya Kalangala.
Mkuu wa mahakama ya kijeshi, Luteni Jenerali Andrew Gutti, amesema kuwa washtakiwa wanaweza kwenda kushiriki vitendo vya vurugu ikiwa watapewa dhamana, hivyo alitupilia mbali ombi hilo.
Wafuasi wengine 13 waliokamatwa na kushtakiwa sambamba na wale wanaoshikiliwa waliachiwa kwa dhamana na masharti mwezi Januari.
Harakati zao zilizuiliwa na walilazimika kulipa dhamana isiyo pesa taslimu ya thamani ya Pauni 3,800. Wadhamini wao waliweka rehani thamani isiyo pesa ya dola13,500.
Ombi la kupatiwa dhamana kwa wafuasi wa Bobi Wine limekuja wakati kukiwa na madai ya kutekwa nyara na kukamatwa kwa wafuasi wa upinzani vitendo vinavyodaiwa kutekelezwa na idara za kiusalama.
Rais Yoweri Museveni siku ya Jumamosi alitupilia mbali ripoti kuhusu utekaji nyara na kusema kuwa vikosi vya usalama watatoa orodha ya wale wanaoshikiliwa.