Mkuu wa Wilaya ya kahama Anna Mringi Macha amepiga marufuku biashara ya nyama ya nguruwe na usafirishaji wa nguruwe wenyewe baada ya wanyama hao kubainika kwa homa ya nguruwe.
Akizungumza na waandishi wa habari, mkuu huyo wa wilaya alisema amechukua uamuzi huo ili kukinga wananchi na watumiaji wa nyama hiyo dhidi ya ugonjwa huo.
“Maeneo yanayofanya biashara ya nyama ya nguruwe, vichinjio, wapishi na sehemu za starehe haziruhusiwi kufanya biashara hiyo kwa sasa mpaka itakapotangazwa tena”-Macha alisema.
Bwana Macha alisema dalili za mlipuko wa ugonjwa huo zilianza Desemba mwaka jana na sasa ni kama unasambaa.
Bwana Macha pia alipiga marufuku usafirishaji wa wanyama hao kutoka sehemu moja hadi nyingine bila kibali cha daktari na atakayekiuka agizo hilo atachukuliwa hatua za kisheria.
Daktari wa Mifugo Halmashauri ya Mji wa Kahama, Dkt. Damian Kilyenyi amethibitisha kuwa zaidi ya nguruwe 500 wamekufa kwasababu ya ugonjwa huo.
Kwa mujibu wa Wataalamu wa afya Homa ya Nguruwe ni ugonjwa wa kupumua unaosababishwa na virusi ya influenza aina A, vinavyofahamika kama H1N1, Chanzo chake ni kwenye nguruwe, lakini sasa huambukiza binadamu na huenezwa kwa kupiga chafya au kukohoa.
Dalili za ugonjwa huo zinakaribiana na za homa ya msimu ambayo dalili zake ni kupata homa kali, kukohoa, maumivu kooni, maumivu mwilini na mzizimo, Na wanaoathirika zaidi huwa ni wajawazito, watoto wa chini ya miaka mitano, wazee wa zaidi ya miaka 65 na wale wenye matatizo mengine ya kiafya.