Saudi Arabia imesema itafungua tena ubalozi wake nchini Qatar katika siku zijazo, kufuatia mkutano wa kilele wa wiki iliyopita ulioungwa mkono na Marekani, ambapo mataifa ya Ghuba yalikubaliana kumaliza mzozo wa miaka mitatu.
Mzozo huo ulianza mnamo mwaka 2017, pale Saudi Arabia, Umoja wa Falme za Kiarabu, Bahrain na Misri zilipoiwekea Qatar vikwazo vya kidiplomasia, kibiashara na vya kusafiri kwa madai kwamba inafadhili makundi ya kigaidi.
Mataifa hayo ya Kiarabu yameahidiana kuimarisha ushirikiano wao, ili kuongeza nguvu ya kupambana na Iran katika eneo la Mashariki ya Kati.
Hayo yakijiri, Marekani kwa mara ya kwanza imezitaja Bahrain na Umoja wa Falme za Kiarabu kama washirika wake wakuu wa usalama, kauli iliyowashangaza wengi.
Halikadhalika, Rais Donald Trump ametunukiwa tuzo ya hadhi ya juu na Mfalme wa Morocco kwa juhudi zake za kurejesha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Morocco na Israel.