Rais wa Uganda Yoweri Museveni anaongoza kwa kura kura nyingi katika matokeo ya awali yaliyotolewa nana Tume ya uchaguziIjumaa asubuhi.
Bw Museveni amepata kura 1,536,205 sawa na (65.02%), huku mshindani wake mkuu Robert Kyagulanyi, maarufu kama Bobi Wine, akipata kura 647,146(27.39%) kutoka vituo 8,310 vya kupigia kura.
Uganda ilikuwa na jumla ya vituo 34,684 vya kupigia kura.
Wakati matokeo hayo yakiarifiwa, imeripotiwa kuwa polisi nchini humo wamevamia hoteli moja ambako kikundi cha wanaharakati wa mashirika ya kiraia na wakaguzi wa uchaguzi walikuwa wamekusanya taarifa kutoka kwa waangalizi wengine wa uchaguzi tofauti na Tume ya uchaguzi.
Msemaji wa polisi nchini humo, Bw Fred Enanga amesema kuwa walipata taarifa za ujasusi kwamba baadhi ya wanaharakati wa kiraia walikuwa wameweka kituo chao cha ukusanyaji wa matokeo ya kura katika Hoteli Africana iliyopo mjini Kampala , kando na kituo cha taifa kinachokusanya matokeo ya uchaguzi wa rais na wabunge.
“Tulituma watu wetu katika Hoteli Africana. Watu wenye jukumu la kudhibiti uchaguzi ni Tume ya uchaguzi. Huwezi kujua ni nini kilicho nyuma ya kituo hiki cha ukusanyaji wa matokeo ya kura. Huenda wana nia mbaya ambayo inaweza kuchochea ghasia . Sheria inaruhusu Tume ya uchaguzi tu kutangaza mataokeo. Kuwa na kituo cha kukusanya matokeo kando kunashusha hadhi ya uchaguzi na tume ya uchaguzi”-Bw Enanga aliiambia NTV Uganda.
Tume ya Uchaguzi nchini Uganda siku ya Alhamisi ilihakikisha kwamba matokeo ya moja kwa moja ya Uchaguzi katika kituo kikuu cha kujumlisha kura cha kitaifa yatendelea licha ya kufungwa kwa intaneti nchini humo.
Chanzo na BBC Swahili.