Rais wa Uganda, Yoweri Museveni amesema kuwa bado hajaona mtu mwenye uwezo wa kuiongoza Uganda kwa sasa, hivyo ataendelea kuwa madarakani.
Museveni mwenye umri wa miaka 76, ameliongoza taifa la Uganda kwa zaidi ya miongo mitatu.
Akizungumza na viongozi wa chama chake cha National Resistance Movement (NRM) hapo jana, amesema kwamba wapinzani wake hawana vigezo vya kuliongoza taifa la Uganda.
"Ninakasirika sana ninaposikia watu wakiniambia niondoke madarakani,”-Museveni alinukuliwa na vyombo vya habari nchini humo.
Na kuongeza kuwa;“ Wapiga kura ndio wanaoamua, hata nikiondoka nani ataweza kuliongoza taifa hili, nitaondoka tu iwapo kuna mtu wa maana nitakayeona naweza kumuachia Uganda".
Rais Museveni ambaye aliingia madarakani kwa njia ya mapigano ya msituni amekaa madarakani tangu mwaka 1986.
Katika uchaguzi mkuu wa Uganda unaotarajiwa kufanyika Januari 14 mwakani una wagombea 11 wa nafasi ya Urais, 10 kati yao wakitaka kuchukua nafasi ya Yoweri Museveni wa chama tawala cha NRM anayetaka kutetea nafasi yake kwa muhula wa sita.