Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amesema Tanzania inahitaji kuwa na kiongozi anayeweza kuunda Serikali na mwenye uwezo wa kupambana na rushwa na mafisadi ambao wanasababisha nchi kukosa maendeleo.
Waziri Majaliwa amesema kiongozi huyo ni lazima awe na uwezo wa kuisimamia Serikali atakayoiunda pamoja na kuhakikisha wateule wake wanatekeleza majukumu yao ipasavyo ikiwa ni pamoja na kuwafuata wananchi waioshio vijijini na kuwatumikia.
Ametoa kauli hiyo leo Jumanne, Oktoba 6, 2020 wakati akizungumza na wakazi wa Kata ya Kirongwe wilayani Mafia, Pwani katika mkutano wa kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM Rais Dkt John Pombe Magufuli pamoja na mgombea ubunge wa jimbo la Mafia Omari Kipanga na wagombea wa udiwani wa CCM.
Amesema hiki ni kipindi muafaka kwa wananchi kuhakikisha ifikapo Oktoba 28 mwaka huu wanajitokeza kwa wingi kwenda kuwachagua viongozi watakaowaletea maendeleo na wasichague viongozi kwa ushabiki ili wasije kujilaumu mwishoni.
Majaliwa amewahakikishia wakazi wa Mafia uwepo wa usafiri kwa muda wote na tayari Serikali imepeleka kivuko kingine kwa ajili ya kuendelea kutoa huduma kati ya Mafia na Nyamisati baada ya kivuko cha awali kuwa kwenye matengenezo.
Wakati huo huo, amesema Serikali itaendelea kujenga barabara za lami nchini zikiwemo na za wilaya ya Mafia na ilianza kwa kujenga barabara zinazounganisha mikoa na sasa inajenga barabara zinazounganisha Wilaya.