Rais wa Marekani Donald Trump anaendelea kupewa uangalizi wa karibu akiwa hospitali ambako anapokea matibabu ya ugonjwa wa Covid-19.
Kuna hali ya wasiwasi kuhusu uwezekano wa Rais Trump kutolewa hospitali,kama walivyokuwa wamesema madaktari wake kwamba huenda akatoka Jumatatu huku maswali yakiibuliwa kuhusu hali yake.
Kiwango cha oksijeni yake kilielezwa kushuka mara mbili na pia anatiliwa tiba ya steroid, Lakini siku ya Jumapili aliushangaza umma alipoonekana hadharani akiendeshwa kwenye gari kuwasalimu wafuasi wake, hatua ambayo ilikosolewa vikali.
Rais Trump, ambaye amekosolewa kwa jinsi alivyoshughulikia na janga la corona, pia alisema amejifunza mengi kuhusu virusi hivyo, Awali madaktari wake walisema Trump anaendelea kupata nafuu na kwamba huenda akatolewa hospitalini leo Jumatatu.
Dk Sean Conley alisema kiwango cha hewa ya oksijeni cha rais kilishuka mara mbili tangu alipogunduliwa kuwa na virusi vya corona, na ameanza kutumia dawa inayofahamika kama dexamethasone.
“Rais aliongezewa oksijeni ya ziada mara moja baada kuthibitishwa kuwa na virusi”- alisema Dk Conley, ambaye pia alifafanua mkanganyiko uliosababishwa na taarifa tofauti kuhusu hali ya Rais Trump.
Kuugua kwa Rais Trump kulikotangazwa hadharani na yeye mwenyewe kwenye mtandao wa Twitter mapema Ijumaa, kumevuruga ratiba yake ya kampeni.
Rais Trump atakabiliana na mpinzani wake wa chama cha Democratic Joe Biden katika uchaguzi wa urais wa Novemba tatu.