Mahakama ya Rufaa ya Tanzania imetupilia mbali uamuzi wa Mahakama Kuu kanda ya Dar es salaam.
Mahakama hiyo iliyokuwa imempa ushindi Dickson Sanga dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali juu ya kufuta baadhi ya vifungu vya sheria ikiwemo kifungu cha 148 (5) cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai ya mwaka 1985 vinavyokinzana na katiba ili kesi zote zikiwemo za utakatishaji fedha na uhujumu uchumi zipate dhamana.
Awali Dickson Sanga, alifungua shauri la madai Mahakama Kuu namba 08 la mwaka 2019 ambapo Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ya Dar es salaam ilimpatia ushindi Mei 18 mwaka huu na kutangaza kuwa kifungu cha 148 (5) cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai ya mwaka 1985 kinakinzana na ibara ya 13(3), 15(1) na 2(a) ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Katika shauri hilo Mahakama Kuu iliiagiza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kurekebisha kifungu hicho ndani ya miezi 18 kutoka siku ya kutolewa kwa hukumu huku ikiionya Jamhuri kuwa kushindwa kufanya hivyo kutasababisha kufutwa kwa kifungu hicho.
Kwa uamuzi uliotolewa na Mahakama Kuu uliompa ushindi Dickson Sanga, uliagiza mabadiliko ya sheria ili kesi zote zinazofikishwa kwenye vyombo vya sheria ziwe na dhamana ikiwemo makosa ya utakatishaji fedha na uhujumu uchumi.
Aidha, kutokana na hukumu hiyo ya Mahakama Kuu, Mwanasheria Mkuu wa Serikali alikata rufaa namba 175 ya mwaka 2020 Mahakama ya Rufaa ya Tanzania ya kupinga hukumu hiyo ambapo rufaa hiyo ilisikilizwa Julai 06 mwaka huu mbele ya Majaji wa Rufaa watano akiwemo Mugasha, Mkuye, Ndika, Mwambegele na Kitusi ambapo hatimaye mahakama hiyo ya rufaa imebatilisha uamuzi huo wa mahakama kuu hii leo Agosti 05.