Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ametia saini kitabu cha maombolezo ya kifo cha aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tatu Mhe. Benjamin William Mkapa kilichotokea jijini Dar es Salaam na ametoa pole kwa familia kwa niaba ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Serikali na amesema serikali pamoja na Watanzania wote wanaendelea kuomboleza kifo cha rais huyo.
Waziri Mkuu ameyasema hayo leo Ijumaa, Julai 24, 2020 nyumbani kwa marehemu Masaki, jijini Dar es Salaam kwa kuwasihi wanafamilia na Watanzania kwa ujumla waendelee kumuombea marehemu kwa Mwenyezi Mungu kwa sababu yote ni mapenzi yake.
“Ndugu wanafamilia, kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali tumepokea taarifa za msiba wa mzee wetu, kiongozi wetu Rais wa Awamu ya Tatu kwa masikitiko makubwa. Nawasihi muendelee kuwa watulivu na wavumilivu katika kipindi hiki kigumu kama alivyosema Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Magufuli.”
Amesema kamati ya mazishi ya Serikali inaendelea na maandalizi pamoja na kuwasiliana na viongozi kutoka katika nchi marafiki ambao marehemu alifanya nao kazi ili kutoa fursa ya wao kushiriki. “Tutatoa taarifa ya ratiba ya kuaga mwili itakayofanyika Uwanja wa Taifa.”
Kufuatia kifo hicho kilichotokea usiku wa kuamkia leo, Rais Dkt. Magufuli ametangaza siku saba za maombolezo ya Kitaifa kuanzia leo Ijumaa, Julai 24, 2020 na katika kipindi chote cha maombolezo bendera zote zitapepea nusu mlingoti.
Aidha, Waziri Mkuu Majaliwa ametangaza ratiba ya mazishi kwa kusema kuwa mwili wa Marehemu Rais Mkapa utazikwa kijijini kwao Lupaso-Mtwara siku ya jumatano ijayo (Julai 29,2020) ambapo mwili huo utasafirishwa kwa ndege siku ya jumanne (Julai 28) baada ya kumaliza shughuli za kuuaga uwanja wa taifa.