Vijana wa Chama Cha Wananchi CUF Mkoa wa Dar es Salaam wamesema wana imani katika wagombea wote wa upinzani ambao wamepitishwa na vyama vyao kuwania nafasi ya Urais hawamuwezi mgombea wa Chama Cha Mapinduzi CCM isipokuwa Mwenyekiti wa Chama hicho Taifa Prof Ibrahim Lipumba.
Mapema asubuhi hii leo vijana hao wamejitokeza katika ofisi ya Wilaya ya Chama hicho Kinondoni ambako anaishi Mwenyekiti wao ambapo kwa kujichangisha wenyewe wameamua kumchukulia fomu na kumkabidhi fomu ya kugombea nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mara baada ya kukabidhiwa fomu hiyo Mwenyekiti wa chama hicho Taifa Prof. Lipumba amesema aliamua kukaa kimya ili kutoa nafasi kwa wanachama wengine wajitokeze kuchukua fomu ili kupambana, Pia yapo mengi ambayo kama Chama wanaamini bado ni matakwa ya wananchi na hayajatekelezwa na serikali.
Prof. Lipumba ameahidi endapo atapata ridhaa atakamilisha mchakato wa uwepo wa Katiba Mpya.
Aidha, kwa mujibu wa chama hicho kesho Julai 24, ndiyo siku ya mwisho ya kurejesha fomu ya wagombea kwa ngazi ya Urais hivyo atalazimika kuijaza fomu hiyo kwa kuwa vijana wa chama hicho wameonesha imani kubwa kwake kuwa anaweza kuwavusha.