Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amemuagiza Katibu Mkuu wa Afya kuwasimamisha kazi mara moja Mkurugenzi wa Maabara ya Taifa ya jamii Dkt. Nyambura Moremi na Bwana Jacob Lusekelo ambaye ni Meneja Udhibiti wa ubora ili kupisha uchunguzi.
Hii ni kufuatia hotuba ya Rais Magufuli aliyoitoa wakati akimuapisha Waziri mpya wa Katiba na Sheria Mwigulu Nchemba hapo jana ambapo alibainisha changamoto za maabara ya Taifa ya Jamii kwa kusema kuwa sampuli kadhaa ambazo hazikuwa za binadamu zilitumwa katika maabara hiyo ili kupima ubora na usahihi wa majibu ya mashine hizo katika vipimo vya ugonjwa huo na baadhi kukutwa ni positive.
Waziri Ummy ameunda Kamati ya wataalam wabobezi kufanya uchunguzi wa mwenendo wa maabara hiyo ikiwemo mfumo mzima wa ukusanyaji na upimaji wa sampuli za COVID-19 na baada ya hapo kuwasilisha taarifa yao kwake kabla ya tarehe 13 Mei,2020.
Kamati hiyo itaongozwa naProf.Eligius Lyamuya kutoka Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) na ndani yake ina wajumbe tisa, sambamba na Uchunguzi wa kamati hiyo, imeelezwa kuwa shughuli za upimaji wa sampuli katika maabara hiyo zitaendelea kama kawaida.