Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ametuma salamu za rambirambi kwa familia ya Wabunge na Waumini wa Kanisa la Mlima wa Moto kufuatia kifo cha Askofu Dkt. Getrude Rwakatare.
Katika salamu za rambirambi rais Magufuli amesema “Katika kipindi hiki cha majonzi, tumuombee Askofu Rwakatare apumzike mahali pema peponi, na nawasihi Waumini wa kanisa la Mlima wa Moto muendelee kuwa wamoja na muendeleze mazuri yote yaliyofanywa na Askofu Rwakatare wakati wa uhai wake”.
Askofu Dkt.Rwakatare alikuwa Mbunge wa Viti Maalumu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Askofu wa Kanisa la Mlima wa Moto (Mikocheni B Assemblies of God) amefariki dunia Alfajiri ya leo Aprili 20.
Kwa mujibu wa mtoto wake Mutta Rwakatare wakati akihojiwa na East Afrika Redio katika kipindi cha Super Breakfast alisema;
"Ni bahati mbaya imetokea asubuhi ya leo saa 11 kasoro, alikuwa na matatizo ya moyo, jana tulimkimbiza Hospitali lakini bahati mbaya imetokea, tupo katika hatua ya kuangalia namna gani tutafanya ili tuweze kumpumzisha mama yetu".
Kupitia mtoto wake huyo amethibitisha ni kweli mama yake amefariki dunia kutokana na presha kupanda.