Msemaji Mkuu wa Serikali na Katibu Mkuu Wizara ya Habari , Dokta Hassan Abbas amesema tayari serikali imepokea Dola Milioni 500 kama mkopo kutoka benki ya dunia ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuendeleza sekta ya elimu.
Dokta Abbas amesema hayo leo Aprili 03, 2020 wakati akihojiwa na kituo hiki cha Star Tv katika kipindi cha Tuongee Asubuhi kenye mada iliyokuwa inaangazia “Ahadi na Uwajibikaji” ambapo amesema kuwa sekta ya elimu kwa Tanzania itaendelea kufanya vyema kupitia mkopo huo.
Amesema Serikali iliomba mkopo kiasi cha Dola 300 lakini fedha waliyoipata kutoka kwa benki ya dunia ni Dola milioni 500 na kusema fedha hizo zitasaidia kutumika pia kwenye maboresho ya miundombinu ya elimu.
Kuhusu suala la watoto wa kike wanaopata mimba pindi wanapaokuwa mashuleni amesema sera zilizokuwepo zitaendelea kuimarishwa na kuboreshwa kwa kuendeleza na msimamo wa serikali uliokuwepo isipokuwa ikitokea mwanafunzi amepatikana na mimba shuleni hatafukuzwa lakini pia hatasoma katika shule aliyokuwa akisomea na badala yake ataenda kusoma katika shule nyingine, lengo likiwa ni kumnusuru mtoto huyo kisaikolojia.
Itakumbukwa kuwa mwezi Juni 2017, Rais Magufuli alitangaza rasmi kuwa wanafunzi watakaopata ujauzito hawataruhusiwa kuendelea na masomo katika shule za serikali na baadaye katika taarifa rasmi iliyotumwa kwa barua pepe na moja ya wasemaji wakuu wa benki hiyo aliyopo jijini London, Benki hiyo ilisema Tanzania imenyimwa mkopo wa Milioni 300 iliyoomba kwa ajili ya elimu na inaendelea na majadiliano na serikali kuhusu ya suala hilo.
Mwisho.