Spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai amesema utaratibu wa maswali na majibu katika bunge la 11 yatajibiwa kwa utaratibu wa maandishi kwa kutumia teknolojia ya simu za viganjani zilizo na mfumo wa kibunge.
Spika wa bunge ametoa kauli hiyo leo Machi 31.03.2020 bungeni jijini Dodoma katika kikao cha kwanza cha bunge ambapo amefafanua kuwa maswali yote yatajibiwa kwa utaratibu wa maandishi kupitia teknolojia ya simu za viganjani ambazo zimebainishwa kuwa zina mfumo wa kibunge na wabunge hao wote watapaswa kuzitumia kwa shughuli hizi za bunge la 11.
Spika Ndugai amesema ikiwa mbunge yeyote atakuwa ana swali la nyongeza kwa wizara husika atapaswa kuandika swali lake na kulituma katika mfumo wa kibunge wa mawasiliano uliobainishwa na Spika ambao amesema ni tofauti na kipindi cha nyuma ambapo majibu yalikuwa yakijibiwa papo kwa papo.
Amesema hakutakuwepo na maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu katika kipindi chote cha mkutano huu wa 19, Pia mawaziri wote wataongelea kwenye meza zao pale walipoketi ndani ya bunge kwa kutumia kipaza sauti (mic) zao vilevile wabunge watapaswa kufanya hivyo pindi watakapokuwa wanauliza maswali kwenye sehemu zao watakazokuwa wameketi pindi walipoingia bungeni na hakutakuwa na mtu atakayetumia kipaza sauti (mic) cha pamoja lengo likiwa ni kufuata ushauri wa kuchukua tahadhari ya ugonjwa wa COVID-19.
Katika utaratibu wa kupiga kura ya Ndio au Sio ili kupitisha bajeti ya mwaka 2020/2021 wabunge watabonyeza kitufe ambacho kitatoa majibu ya jumla ya kura hizo za bajeti zilizopigwa na wabunge hao waliohudhuria kikao cha bunge.
Kikao cha kwanza cha bunge la 11 kimeanza leo ikiwa ni mkutano wa 19 ambapo mbali na Spika Ndugai kutoa utaratibu wa bunge litakavyokuwa linaendeshwa alitumia wasaha kwa kuwasihi wabunge kuchukua tahadhari za ugonjwa unaoambukizwa na virusi vya Corona, huku kikao cha pili kikitazamiwa kuanza kesho saa nane kamili mchana.
Mwisho.