Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam imemhukumu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA Freeman Mbowe na wenzake kulipa faini ya Shilingi Milioni 350 ama kwenda jela miezi 5 baada ya kupatikana na hatia kwenye makosa 12 likiwemo la kufanya maandamano.
Hukumu hiyo iliyochukua takribani saa 4, kuanzia saa 7 mchana hadi saa 11 jioni, imetolewa na Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba baada ya kusikiliza ushahidi wa mashahidi 23 baina ya utetezi na Serikali.
Katika hukumu hiyo, Hakimu Simba amesema amewatia hatiani washitakiwa katika mashitaka 12 kati ya 13.
Kosa ambalo hawajatiwa nalo hatiani ni kosa la kwanza ambalo ni kufanya mkusanyiko usio halali.
Hakimu Simba amesema mashitaka waliyotiwa hatiani ni mabaya katika jamii ukizingatia wao ni viongozi na walitakiwa kuwa mstari wa mbele katika utii wa sheria, hivyo mahakama inaona kuwa wanastahili adhabu kali ili iwe fundisho kwa wengine watakaofanya makosa kama hayo,
Hakimu Simba amesema atatoa adhabu kali lakini kwa kuzingatia hoja ya kuwa washitakiwa ni wakosaji wa kwanza na wanatakiwa kupewa huruma na ukizingatia wengine walishakaa mahabusu, hivyo kukaa kwao ndani ni adhabu tosha kwa mantiki hiyo anawaepusha na adhabu ya vifungo kwa washitakiwa wote,
Katika adhabu hiyo, Mbowe amehukumiwa kulipa Sh. Milioni 70, Halima Mdee Sh.Milioni 40, Dr.Mashinji kulipa Sh.Mililioni 30, John Heche Sh.Milioni 40, Msigwa Sh.Milioni 40, Bulaya Sh.Milioni 40, Mnyika Sh.Milioni 30, Salum Mwalimu Sh.Milioni 30 na Ester Matiko Sh.Milioni 30.
Awali Wakili Kibatala amemwomba Hakimu kutoa hukumu ya washtakiwa walipe faini badala ya kuwapa adhabu ya kifungo baada ya washtakiwa wote kukutwa na Hatia kwenye makosa 12 kati ya makosa 13 yaliyokuwa yanawakabili.
Katika kesi hiyo Serikali ilifunga ushahidi kwa kuita mashahidi wanane huku upande wa utetezi ukiita mashahidi 13 wakiwemo washtakiwa wenyewe.
Katika kesi hiyo namba 112 ya mwaka 2018 washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka 13 ikiwemo kula njama, kufanya mkusanyiko usio halali kati ya Februari 1 na 16, 2018 katika Viwanja vya Buibui na Barabara za kawawa na Mkwajuni, Kinondoni jijini Dar es Salaam wakati wa kampeni za uchaguzi mdogo wa Jimbo la Kinondoni.
Mwisho