Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imepanga machi 10, 2020 kutoa hukumu ya kesi inayowakabili viongozi nane wa chama cha demokrasia na maendeleo chadema akiwemo mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe.
Mshtakiwa mwingine katika kesi hiyo ni Dkt. Vicent Mashinji ambaye alikuwa Katibu Mkuu wa zamani wa CHADEMA na kwasasa amehamia CCM mnamo februari 18, 2020.
Katika kesi hiyo namba 112 ya mwaka 2018 washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka 13 ikiwemo kula njama, kufanya mkusanyiko usio halali kati ya februari 1 na 16, 2018.
Uamuzi huo umetolewa na Hakimu Mkazi Mkuu Thomas Simba.
Pia Mahakama hiyo imetoa siku tano kwa mawakili wa pande zote kuwasilisha majumuisho kwa njia ya maandishi.
Hakimu Simba amesema kwa mujibu wa sheria ya uendeshaji wa mashauri ya jinai pande zote zitakuwa na haki kisheria kuomba kufanya majumuisho ili kuweza kusaidia mahakama kutoa uamuzi wake
Hakimu Simba amebainisha kuwa mahakama inaendelea kuchapa mwenendo mzima wa kesi toka ilipoanza kwa ajili ya kukabidhi kwa pande zote mbili.
Katika kesi hiyo serikali ilifunga ushahidi kwa kuita mashahidi wanane huku upande wa utetezi ukiita mashahidi 13 wakiwemo washtakiwa wenyewe.
Mbali na Mbowe na Dkt.Mashinji, washtakiwa wengine ni Katibu Mkuu wa chadema, John Mnyika; Naibu Katibu Mkuu Salum Mwalimu (Zanzibar) na mbunge wa Iringa mjini, Mchungaji Meter Msigwa.
Pia wengine ni Mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko; Mbunge wa Kawe, Halima Mdee; Mbunge wa Bunda, Esther Bulaya; Mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche.
Mwisho