Upande wa mashtaka katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili mwandishi wa Habari za uchunguzi Erick Kabendera umeieleza Mahakama ya hakimu Mkazi Kisutu kuwa mchakato wa makubaliano kati ya Kabendera na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) bado unaendelea.
Habari na Angela Mathayo.
Wakili wa Serikali, Gloria Mwenda ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya Hakimu Mkazi Janet Mtega kuwa majadiliano kati ya ofisi ya mkurugenzi wa mashtaka (DPP) na mwandishi wa habari za uchunguzi, Erick Kabendera bado unaendelea.
Mwenda amesema kesi hiyo imekuja kwa ajili ya kutajwa kwa kuwa upelelezi haujakamilika.
Katika maelezo yake, Mwenda amesema kuwa majadiliano kati ya mshtakiwa na DPP bado yanaendelea, kuiomba mahakama kuipangia kesi hiyo tarehe nyingine.
Baada ya maelezo hayo, Hakimu Mtega ameahirisha kesi hiyo hadi Februari 10 mwaka huu kwa ajili ya kutajwa tena.
Katika kesi hiyo, Kabendera anakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi yenye mashtaka matatu likiwemo la utakatishaji wa Sh.Mil 173.
Kwa mara ya kwanza Kabendera alifikishwa mahakamani hapo Agosti 5, 2019 akikabiliwa na makosa hayo anayodaiwa kuyafanya kati ya Januari 2015 na Julai 2019, jijini Dar es Salaam.
Mwisho