Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inafanya juhudi kuendeleza miradi ya maji safi na salama ambayo itawezesha changamoto ya upatikanaji wa huduma hiyo kuwa historia.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameyasema hayo leo katika hotuba yake wakati wa ufunguzi wa Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira wa Mkoa wa Mjini Magharibi (ZUWSP)-ADF 12 huko Saateni Wilaya ya Mjini Unguja ikiwa ni shamrashamra za miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Rais Dk. Shein amesema kuwa huduma za maji safi na salama kabla ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 zilikuwa zikitolewa kwa ubaguzi licha ya kuwa ni neema aliyoileta MwenyeziMungu kwa waja wake.
“Matumaini yangu ni makubwa kwa mradi huu, fedha zote lengo lake ni kuhakikisha kwani mikakati kabambe yakuimarisha miradi ya maji imeaanza natumai awamu zijazo zitaendeleza mikakati hiyo kwa azma ya kuwapatia wananchi huduma hii muhimu hapa nchini, nasisitiza kuwa maji hayauzwi hapa Zanzibar bali yanachangiwa”.
Alisema kuwa kwa Zanzibar wakati huo huduma zote muhimu zilianza katika nyumba za mawe zilizokuwepo katika eneo la mji mkongwe pekee yake.
Rais Dk. Shein alieleza umuhimu wa maji kwa wanaadamu, wanyama na miti na kueleza kuwa ndio maana serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikafanya juhudi za makusudi kuhakikisha huduma hiyo inaimarika hasa ikizingatiwa kuwa maji hayana mbadala.
Aidha, Rais Dk. Shein ameeleza jinsi ya Washirika wa maendeleo wakiwemo nchi rafiki ikiwemo Ras al Khaimah, Sharja, Japan, China, India na wengineo walivyoiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maji.
Mara baada ya kuwasili katika eneo la Saateni, Rais Dk. Shein amepata maelezo juu ya mradi wa maji kwa tanki la Saateni na tanki la mnara wa mbao kutoka kwa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) Mussa Ramadhan Haji.
Akisoma taarifa ya kitaalamu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati Ali Halil Mirza ameipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein kwa uongozi wake mahiri kwa kuamua kutekeleza Mradi wa Maji na Usafi wa Maziringira wa Mkoa wa Mjini Magharibi.
“Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba,Maji na Nishati inatarajia mradi huu utaendeshwa na kutunzwa vizuri kwa ushirikiano kati ya mamlaka ya maji Zanzibar, tujitahidi kuutunza.”-Ali Halil Mirza-Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati.
Mwisho.