Kijana Devenja Kibotuo (35) mkazi wa Kijiji cha Uchau kusini Wilaya ya Moshi,mkoani Kilimanjaro anadaiwa kufukua kaburi la mtoto wa dada yake aliyezikwa miaka 16 iliyopita kisha kuotesha mgomba kwenye kaburi hilo.
Kijana huyo anadaiwa kufukua kaburi la mtoto wa dada yake aitwae Juliana Andrea aliyezikwa mwaka 2004 ambae alifariki akiwa na umri wa miezi tisa huku tukio hilo likihusishwa na imani za kishirikina.
Wahenga walisema damu nzito kuliko maji ila kwa kijana huyu imekuwa kinyume,tukio hilo ambalo limezua sintofahamu baada ya ndugu kujua kaburi limefukuliwa wanasema walikuta sanda ikiwa juu ya kaburi huku wakikosa majibu kutoka kwa ndugu yao aliyefukua kaburi kisha kupanda mgomba.
Mmoja wa wana familia alieleza kuwa kwa mila na taratibu zao inapotokea kaburi limefukuliwa ni lazima zifanyike mila kwa ajili ya kulifukia na endapo haitafanyika hivyo itakuwa na madhara kwa familia.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoani Kilimanjaro James Manyama amethibitisha kumshikilia kijana Devenja baada ya kufukua kaburi hilo mtoto wa dada yake bila kuwa na kibali cha mahakama.
Jeshi la polisi kutoka mkoani humo limesema litafukua kaburi hilo siku ya leo jumatatu baada ya kupata kibali cha mahakama ili kujua kama kuna masalia ya mifupa itakuwa imechukuliwa na kijana huyo pamoja na kushirikisha idara ya afya kujua kama kijana aliyefukua kaburi hilo ana akili timamu.
Mwisho