Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Pombe Magufuli ametunukiwa shahada ya heshima ya udaktari wa falsafa katika sayansi kwenye ukumbi wa Chimwaga uliopo Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM)
Kiongozi mkuu huyo wa nchi ametunukiwa shahada hiyo leo Alhamisi Novemba 21, 2019 katika mahafali ya 10 ya chuo hicho ambapo mkuu wa chuo hicho Rais mstaafu, Benjamin Mkapa naye amehudhuria katika mahafali hayo.
Viongozi waliohudhuria mahafali hayo ni Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai, mawaziri kutoka wizara mbalimbali pamoja na wabunge.
Makamu Mkuu wa chuo hicho, Profesa Faustine Bee amesema shahada hiyo inatolewa kwa Rais Magufuli kutokana na uongozi wake katika ujenzi wa uchumi wa viwanda, kuwekeza katika elimu, miundombinu, mawasiliano, nishati, utalii na kuimarisha utawala bora pamoja na mapambano dhidi ya rushwa.
Prof. Faustine amesema shahada hiyo imewahi kutolewa kwa Rais mstaafu Jakaya Kikwete mwaka 2010 na pia waziri mkuu wa zamani marehemu Rashid Kawawa ambapo Rais Magufuli ni kiongozi wa tatu kutunukiwa shahada katika chuo cha UDOM.
Wahitimu 6,488 watatunukiwa astashahada, shahada, stashahada ya juu, shahada ya umahiri na shahada ya uzamivu.
Mwisho