Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kasim Majaliwa, amewataka wakuu wa polisi kutoka nchi kumi na nne zinazounda shirikisho la EAPCO kuweka mikakati itakayo saidia nchi zao kukabiliana na tatizo la uhalifu unaovuka mipaka ikiwemo wimbi la biashara ya madawa ya kulevya ,utakatishaji wa fedha, bidhaa bandia na usafirishaji wa binadamu.
Akifungua mkutano wa ishirini na moja wa shirikisho la wakuu wa polisi mashariki mwa Afrika kwa niaba ya Raisi wa jamuhuri ya muungano wa Tanzania John Pombe Magufuli ,waziri mkuu amesema bado nchi wananchama zinakabiliwa na uhalifu kwa kukosa sheria moja katika kukabilina na wahalifu. Waziri mkuu ameeleza kuwa ili jitihada zinazo fanywa na wakuu wa majeshi ya polisi ziweze kufanikiwa utashi wa kisiasa unahitajika ili kuvipa nguvu vyombo vya dola katika kutekeleza majukumu yao . Kufunguliwa kwa mkutano huu kunatoa fursa ya Tanzania kuwa mwenyekiti mpya wa shirikisho hilo kupitia kwa mkuu wa jeshi la polisi Simon Sirro . Mwenyekiti mpya wa EAPCO Simon Sirro na mwenyekiti aliyemaliza muda wake Luthen Generali Adil Mohamedi kutoka Sudan wanawaomba wakuu wa majeshi ya polisi kutoa ushirikiano kwao ili kufikia malengo kusudiwa katika kukabiliana na uhalifu unaovuka mipaka. Hii ni mara ya pili kufanyika kwa mkutano huu tangu ulipofanyika kwa mara ya mwisho mwaka 2002 ukiwa ni utaratibu wa kawaida wa shirikisho hilo kufanya mkutano katika nchi inayopokea uwenyekiti.