Serikali wilayani Chunya mkoani Mbeya imethibitisha kuwepo kwa vitendo vya udhalilishaji na ukatili dhidi ya wanawake wakulima wawapo mashambani vinavyotekelezwa na wafugaji.
Kati ya matukio yaliyoripotiwa Ofisini kwa mkuu wa wilaya ni pamoja na wanawake wakulima kubakwa na kupigwa na wafugaji wakilenga kuwaondoa ili waingize mifugo na kuilishia kwenye mazao mashambani.Kufuatia hali hiyo, Mkuu wa wilaya ya Chunya Marypriscar Mahundi ametoa onyo kali kwa wakulima walio na tabia hiyo akisema hatosita kuchukua hatua kali kumwajibisha yeyote atakayebainika kuendeleza vitendo hivyo vya kikatili. Kwa mujibu wa mkuu huyo wa wilaya kata ambazo zimekuwa na wafugaji wenye tabia za kuwanyanyasa wanawake wakiwa mashambani ni pamoja na kata ya Upendo ,Mamba na Lualaje zilizo na wafugaji wengi.
Aidha mkuu huyo wilaya amesema kuwa endapo vitendo hivyo vya udhalilishaji na vipigo kwa wanawake vitaendelea hakutakuwa na maana ya kuwepo kwa jukwaa la wakulima na wafugaji ambalo kazi yake ni kuwatetea watu wa pande zote.
Hata hivyo Katibu wa chama cha wafugaji Wilayani Chunya ,James Kidayi akizungumzia suala la wafugaji kuwafanyia ukatili wanawake mashambani amesema hajawahi kupata taarifa zozote kama viongozi wa chama cha wafugaji. Mwakilishi wa mkuu wa Polisi wilaya ya chunya ,Janeth Mwakabungu amewataka wafugaji kuacha tabia ya kutembea na fimbo mikononi akisema inachangia kufanya ukatili wakati wowote wanapojisikia kufanya hivyo.