Jukwaa la wadau wa kilimo nchini ANSAF limefanya zoezi la ufuatiliaji wa uwajibikaji jamii wilayani Ukerewe kwa lengo la kuangalia kama michakato ya kupanga, kutekeleza na kusimamia rasilimali za umma zinafanyika kwa kuzingatia sheria na miongozo ya serikali za mitaa.
Hayo yamezungumzwa wakati wa kupokea matokeo ya uchambuzi wa ufuatiliaji na uwajibikaji jamii Huku Mkuu wa wilaya ya Ukerewe Cornel Magembe, akisema ushirikishaji jamii katika shughuli za maendeleo utafungua ukurasa mpya katika Nyanja mbalimbali za maendeleo ikiwemo uvuvi. Kwa upande wake Edina Lugano kwa niaba ya mkurugenzi wa ANSAF Audax Lukonge, amesema ushirikishwaji jamii utaongeza ushawishi wa jamii kushiriki katika maswala ya maendeleo hatimaye kunufaika na rasilimali zilizopo. Jumla ya wilaya 34 nchini zimefikiwa na Jukwaa la wadau wa kilimo Tanzania ANSAF katika kuendesha zoezi la ufuatiliaji na uwajibikaji jamii ili kuongeza uwazi na uwajibikaji kwa kushirikisha jamii katika kujiletea maendeleo ambapo mambo mbalimbali ya maendeleo yamejadiliwa na kutafuta ufumbuzi wa changamoto zilizobainika.