Wilaya ya Sengerema Mkoa wa Mwanza imeanzisha mchakato wa kuwakamata vijana wanaoonekana na wanafunzi wa kike katika vichochoro ama maeneo mengine yanayotia mashaka ya mahusiano ili kunusuru vijana na kadhia ya kupata ujauzito.
Akizungumza na wazazi pamoja na walezi wa watoto waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano katika shule ya sekondari ya Nyehunge, Mkuu wa wilaya ya Sengerema Emmanuel Kipole ameahidi kulisimamia suala la watoto wa kike kupata ujauzito katika umri mdogo, jambo ambalo linawanyima nafasi ya kupata masomo.
Amewataka wazazi na walezi kushiriki moja kwa moja katika malezi ya vijana wao wa jinsi zote Ili kutoa fursa ya wanawake kushika madaraka, baada ya kupata elimu. Shule ya sekondari Nyehunge iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa inaanzisha masomo ya kidato cha tano na sita ili kutoa nafasi pana kwa vijana kuifikia elimu ya juu, ingawa bado inakabiliwa na changamoto kadhaa.
Shule ya Sekondari Nyehunge imepokea wanafunzi wa chaguo la pili katika Tahasusi za CBG na HGL wakiwa wavulana 42 na wasichana 39, wanafunzi walioripoti hadi sasa ni 65 sawa na asilimia 80.
Picha na mtandao