Makamu wa Rais wa Tanzania amemuagiza Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tamisemi Dkt. Festo Dugange kumsimamisha kazi Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu Hamis Dambaya ili kupisha uchunguzi kutoka vyombo husika.
Dkt. Mpango, amefika uamuzi huo leo Julai 24, 2021 mara baada ya kufanya ziara ya kushtukiza katika stendi ya Mabasi ya Mangaka iliopo Wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara.
Makamu wa Rais amekasirishwa na uongozi wa Wilaya kufanya upotevu wa fedha usiolingana na matokeo ya ujenzi wa mradi huo.
Ujenzi wa majengo ya stendi hiyo umetumia Shilingi Bilioni 2.2 kiasi ambacho Makamu wa Rais amesema hakilingani na ujenzi huo.
“Unajua vitu vingine Mkurugenzi ukiona huwezi kazi hii awamu ya sita jiondoe mwenyewe, Kwasababu hili jengo la hii stendi halijatumia hizo zaidi ya Shilingi Bilioni mbili unazonitamkia....lakini nitakufuatilia mpaka hela ipatikane…alafu unasema uongo na hela za maskini hawa. Hizo hela zirejeshwe kwasababu kinachooneka ni wakandarasi wanachezea hili jengo, anza kushughulika naye”- Ameagiza Makamu wa Rais Dkt. Mpango.
Aidha, Dkt. Mpango amesema viongozi hawana budi kusimamia fedha za serikali zinazopelekwa katika maeneo yao ili kuwaletea maendeleo wananchi na si vinginevyo.