Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imesema itafungua rasmi dirisha la awamu ya pili ya udahili wa shahada ya kwanza kwa mwaka wa masomo 2020/2021 Novemba 12 mwaka huu.
Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es salaam Katibu Mtendaji TCU Prof.Charles Kihampa amesema awamu hiyo ya pili ya udahili wa shahada ya kwanza itaanza rasmi Novemba 12,2020 na kukamilika Novemba 18 mwaka huu.
Amesema kufunguliwa kwa awamu hiyo ya pili ni fursa kwa waombaji ambao hawakuweza kutuma maombi ya udahili au kudahiliwa katika awamu ya kwanza kutokana na sababu mbalimbali hii ndo nafasi yao.
“Tunasisitiza kwa waombaji ambao hawakuweza kutuma maombi ya udahili au kudahiliwa kuitumia fursa hii kutuma maombi yao ya udahili katika vyuo wanavyopenda”-amesema Prof.Kihampa.
Prof.Kihampa amesema Taasisi za Elimu ya juu zinapaswa kutangaza programu ambazo bado zina nafasi ili waombaji waweze kutuma maombi, Huku akisisitiza kuwa waombaji wanapaswa kuzingatia utaratibu wa udahili kwa awamu ya pili kama ilivyooneshwa katika kalenda ya udahili iliyotolewa na TCU.
Aidha amewataka waombaji udahili wa shahada ya kwanza kuzingatia kuwa Masuala yanayohusu udahili au kujithibitisha katika chuo kimoja yawasilishwe moja kwa moja katika Vyuo husika..
Prof. Kihampa amebainisha kuwa waombaji waliodahiliwa katika chuo zaidi ya kimoja wanapaswa kudhibitisha udahili wao katika chuo kimojawapo kuanzia Sasa hadi Oktoba 17 mwaka huu.
Awamu ya kwanza ya udahili kwa ngazi ya shahada katika Taasisi za Elimu ya juu kwa mwaka wa masomo 2020/2021 umekamilika ambapo majina yanatarajia kutagazwa na vyuo husika.