Rais wa Marekani Donald Trump amesema ni heshima kuwa Marekani ina idadi kubwa ya maambukizi ya virusi vya corona duniani.
Trump alisema''Ninalitazama suala hili kama heshima fulani, kama jambo zuri kwasababu inamaanisha kuwa vipimo vyetu viko vizuri”.
Kwa mujibu wa takwimu zinazokusanywa na Chuo Kikuu cha Johns Hopkins kimeeleza kuwa Marekani ina watu milioni 1.5 walioathiriwa na virusi vya corona na karibu vifo 92,000 vimeripotiwa.
Kwa mujibu wa kituo cha kupambana na kudhibiti magonjwa , Marekani imepima watu milioni 12.6 mpaka siku ya Jumanne.
Kamati ya uongozi ya kitaifa ya chama cha Democratic imekosoa kauli ya Trump, ikisema kwenye ukurasa wake wa Twitter kuwa kuwa na waathirika wa Covid-19 milioni 1.5 nchini Marekani kunaonesha ''kushindwa kabisa kwa uongozi'' na sio sahihi kusema ni heshima.
Aidha, Marekani pia imeripoti vifo vingi vinavyotokana na ugonjwa huo kuliko nchi nyingine yoyote, ingawa kwa ulinganifu wa idadi ya watu na vifo Marekani ni ya sita nyuma ya Ubelgiji, Uingereza na Ufaransa na hii ni kwa mujibu wa takwimu za Chuo cha Johns Hopkins