Maafisa watano wa polisi wamefariki na watu wengine 40 kujeruhiwa baada ya gari moja kugonga katika gwaride katika jimbo la Wisconsin.
Picha zilizochapishwa mtandaoni zinaonesha gari jekundu aina ya SUV likipelekwa katikati ya umati wa watu katika mji wa Waukesha, magharibi mwa jimbo la Milwaukee mwendo wa saa kumi na dakika 40.
Mkuu wa polisi Dan Thompson alisema gari hilo liligonga makumi ya watu ikiwemo Watoto.
Mtu mmoja tayari amekamatwa na kisa hicho 'hakionekani kuwa tukio la ugaidi wakati huu’, maafisa wamesema.
Afisa wa polisi aliyechunguza kisa hicho aliambia washirika wa BBC nchini Marekani CBS News kuwa Mshukiwa alionekana kutoroka.
Mkazi Angelito Tenoria aliambia gazeti la Milwaukee Sentinel kwamba alikuwa ametoka kushiriki katika gwaride hilo wakati tukio hilo lilipotokea.
"Tuliona gari aina ya SUV …likiendeshwa kwa kasi kuelekea njia ambayo gwaride hilo lilikuwa likifanyika na baadaye tulisikia kishindo kikubwa huku kelele za watu waliogongwa na gari hilo zikisikika’’, Alisema Tenoria.
Corey Montinho alisema kwamba kikosi cha wachezaji densi wa mwanawe waligongwa na gari hilo.