Kundi la jeshi linaloshikilia madarakani nchini Mali limetoa nafasi kwa ujumbe wa Umoja wa Mataifa kukutana na rais Ibrahim Boubacar Keïta na kuchukua hatua ya kuwaachilia huru wafungwa wawili kabla ya ujumbe wa Jumuiya ya Kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS kuwasili jijini Bamako Jumamosi.
ECOWAS inataka rais Ibrahim Boubacar Keita na viongozi wengine wanaoshikiliwa na jeshi waachiliwe huru na taasisi za serikali zilizokuwepo zirejeshwe kwenye nafasi zao.
Ujumbe wa Jumuiya ya Kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi (ECOWAS) utaongozwa na rais wa zamani wa Nigeria Goodluck Jonathan, ambaye ataongozana na rais wa Tume ya ECOWAS, Jean-Claude Kassi Brou, na Waziri wa Mambo ya Nje wa Niger, Kalla Ankourao, vyanzo kutoka jumuiya hiyo vimebaini.
Kundi la wanajeshi lililofanya mapinduzi limesema liko tayari kupokea ujumbe wa ECOWAS kesho Jumamosi, mmoja wa viongozi wa kundi hilo la wanajeshi ameliambia shirika la habari la AFP.
Hata hivyo ishara ya kundi hilo la wanajeshi linalodai kwamba linataka kuunda serikali ya mpito ya muda mfupi, inakuja wakati upinzani umeitisha maandamano makubwa leo Ijumaa jijini Bamako "kusherehekea ushindi wa raia wa Mali", siku tatu baada ya rais Keïta, madarakani tangu 2013, kutimiliwa mamlakani.
Alhamisi jioni, wanajeshi waliofanya mapinduzi waliruhusu timu ya Umoja wa Mataifa kukutana na viongozi wanaoshiliwa, ikiwa ni pamoja na rais aliyepinduliwa madarakani IBK na Waziri wake Mkuu Boubou Cissé.