Rais wa zamani wa Afrika Kusini Jacob Zuma, aliyetakiwa kujisalimisha gerezani ili kukitumikia kifungo cha miezi 15 kwa kuupuza amri ya Mahakama, amesema hatotii hukumu hiyo.
Wiki iliyopita, Mahakama ya Katiba ilimpa adhabu hiyo rais Zuma, kwa kutoheshimu agizo la Mahakama kutoa ushahidi kwa Tume iliyokuwa inachunguza madai ya ufisadi alipokuwa rais kati ya mwaka 2009 hadi 2018.
Akizungumza katika mkoa wa Kwa-Zulu Natal alikozaliwa, Zuma amewafananisha Majaji walitoa hukumu dhidi yake kama viongozi waliongoza taifa hilo wakati wa kipindi cha mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi.
Kiongozi huyo amesema kumtaka aende jela kwasasa ni sawa na kumpa hukumu ya kifo; "Hakuna haja ya mimi kwenda jela, kunifunga katika kipindi hiki, kwa umri wangu, ni sawa na kunipa hukumu la kifo"- Alisema Zuma.
Zuma mwenye umri wa miaka 79, alipaswa kujisalimisha gerezani siku ya Jumapili wiki iliyopita, lakini Mahakama imekubali kusikiliza rufaa ya kupinga kifungo hicho cha miezi 15.
Aidha wafuasi wa Zuma wameapa kutokubali kiongozi wao huyo wa zamani kufungwa.