Rais wa Uganda Yoweri Museveni ametangaza masharti zaidi ya kukabiliana na kuenea kwa virusi vya corona wiki mbili baada ya kupiga marufuku usafiri wa Umma.
Hayo yamejiri katika hotuba yake kwa taifa lake kwenye televisheni ambapo usiku wa Jumatatu Rais Museveni amepiga marufuku usafiri wa kutumia magari binafsi na bodaboda kuanzia saa nne usiku.
Rais Museveni amesema mtu yeyote atakayehitaji huduma za dharura za kiafya kama vile kujifungua au kufanyiwa upasuaji atatakiwa kupata idhini kutoka kwa maafisa wa serikali katika ngazi ya Wilaya kabla ya kutoka nyumbani
Aidha, wauzaji wa bidhaa za chakula sokoni watahitajika kuondoka maeneo yao ya biashara hadi pale serikali itakapokamilisha kushughulikia maeneo mapya ya wao kuuzia bidhaa zao.
Rais Museveni pia ameahidi msaada wa chakula kwa watu ambao hawafanyi kazi kutokana na vikwazo vya kukabiliana na COVID-19 na hawana uwezo wa kujipatia bidhaa hiyo muhimu.
Mpaka kuifikia sasa Uganda imethibitisha kuwa na wagonjwa 33 wa corona na maafisa wanatarajia idadi hiyo kuongezeka na hakuna vifo vilivyoripotiwa mpaka sasa.
Magari binafsi yatazuiwa kuingia barabarani baada ya maelekezo ya awali kutaka magari kubeba abiria watatu pekee kukiukwa, na baadhi ya watu kutumia magari binafsi kuwasafirisha wengine na kuongeza hatari ya kusambaa kwa virusi hivyo. Limeandika gazeti la New vision la Uganda.
Rais Museveni amesema kuwa siku 14 zitatumika kubaini, kuwafuatilia na kuwatenga wale wote waliokaribiana na watu waliothibitishwa kuwa na maambukizi ya virusi vya corona.
Kati ya nchi 54 barani Afrika, ni nchi 10 tu mpaka kufikia sasa hazijathibitisha kuwa na maambukizi ya ugonjwa wa COVID-19.
Gazeti la Daily Monitor la Uganda limeandika kuwa Museveni ameamuru kufungwa kwa maduka makubwa, maduka ya vifaa, biashara zisizo za chakula, saluni, nyumba za kulala wageni na karakana za magari kwa siku 14, ambapo maeneo hayo yamesemekana hukusanya watu wengi, Amri hiyo haitahusu hospitali, maeneo yanayotoa huduma za kitabibu na mashirika yanayojihusisha na masuala ya afya.
Mwisho