Waziri wa afya nchini Kenya Mutahi Kagwe amethibitisha kisa cha mtu mmoja kutoka nchini humo kuugua ugonjwa wa Corona katika tangazo alilolitoa moja kwa moja kupitia vyombo vya habari.
Waziri Mutahi amesema kwamba mtu huyo mwenye maambikizi ya virusi vya Corona alithibitishwa kuwa ana maambukizi hayo Alhamisi usiku Machi 13,2020.
Waziri huyo amesema kisa hicho ni cha kwanza kuripotiwa nchini Kenya tangu kuzuka kwa mlipuko wa ugonjwa huo mjini Wuhan nchini China mwezi disemba mwaka jana.
Kisa hicho ni cha raia wa Kenya aliyewasili nchini humo kutoka Marekani kupitia mjini London nchini Uingereza tarehe 5 mwezi Machi 2020.
Mgonjwa huyo aligunduliwa kuwa na virusi hivyo katika maabara ya wizara ya afya nchini Kenya, huku Waziri huyo akisema kwamba mgonjwa huyo ambaye ni mwanamke yuko katika hali njema na kwamba viwango vyake vya joto vimeshuka na kuwa vya kawaida.
Aidha, Waziri Kagwe amewataka Wakenya kuwa watulivu na kuacha wasiwasi kwani serikali ya Kenya kupitia wizara ya afya itaendelea kuimarisha mikakati ili kuhakikisha kwamba hakuna usambazaji wa virusi hivyo zaidi.
Kamati ya dharura ilioanzishwa ili kukabiliana na kuenea kwa virusi vya corona itaendelea kutoa muongozo ili kukabiliana na ugonjwa huo hatari.
Amewahakikishia Wakenya kwamba Kenya imejiandaa vizuri ili kukabiliana na virusi hivyo tangu kisa cha kwanza kitangazwe nchini China, akiongezea kuwa serikali itatumia raslimali zake zote kukabiliana na janga hilo.
Waziri Kagwe amesema kwamba Kenya inaelekea katika wakati ambapo sekta za kibinafsi na zile za kibiashara zitalazimika kuisaidia serikali na raia katika kuchukua jukumu la kukabialana na janga hili.
Mwisho.