Wanafunzi saba wamekufa na wengine 57 wamejeruhiwa baada ya jengo la darasa moja kuanguka katika shule moja ya msingi katika mji mkuu wa Kenya, Nairobi.
Msemaji wa serikali ya Kenya, Kanali Cyrus Oguna, amewaambia waandishi habari kwamba jengo hilo limeanguka mapema leo asubuhi katika shule ya Precious Talent Academy kwenye eneo la Dagoretti. Majeruhi wa kwanza waliondolewa na kupelekwa katika zahanati ya Kanisa Katoliki iliyo karibu na shule hiyo kwa kutumia pikipiki, kwa sababu magari ya kubeba wagonjwa yalifika baada ya saa moja. Shirika la Msalaba Mwekundu limeandika katika mtadao wake wa Twitter kwamba limefungua dawati la kutoa taarifa na litatoa msaada wa huduma za kisaikolojia. Mkuu wa shule hiyo, Moses Wainaina Ndirangu amesema huenda jengo hilo limeanguka kutokana na ukarabati unaoendeleza katika mifumo ya maji taka kwenye upande mmoja wa madarasa.
CHANZO: Idhaa ya Kiswahili DW