Wizara ya afya nchini imetangaza kwamba uchunguzi wa serikali uliokuwa ukifanywa katika maabara kuu ya nchi hiyo umebaini kuwa moja ya mashime ya kupima corona ilikuwa na hitilafu.
Waziri Ummy Mwalimu hii leo ametangaza matokeo ya uchunguzi aliyoagiza kufanyika baada ya Rais wa Tanzania John Pombe Magufuli kutilia shaka ufanisi wa maabara hiyo.
Waziri wa Afya Ummy amesema;"Kamati imebaini kuwepo kwa mapungufu ya uendeshaji wa kitaaluma katika upimaji wa vipimo na uhakiki wa ubora wa majibu''
Licha ya hitilafu hiyo kupatikana pia kumebainika kuwepo kwa udhaifu katika uhifadhi wa vipimo vya covid-19, pamoja na upungufu wa Wataalamu.
Wizara ya afya nchini imeweka wazi kwamba sasa vipimo vitakuwa vinafanyika katika maabara iliyopo Mabibo ambayo ina vifaa vya kisasa vyenye ubora na uwezo wa kupima sampuli 1,800 ndani ya saa 24.
Kwa mujibu wa Waziri Ummy amesema maabara iliyotumika awali na kukutwa na mapungufu ilikuwa na uwezo wa kupima sampuli 300 kwa saa 24 na ilianzishwa mwaka 1968 katika ofisi za NIMR, mtaa wa Obama DSM, na sasa imeamamrishwa kupima magonjwa mengine.